Nini Najsi?
Kilugha ni kila uchafu, kisharia
ni uchafu wenye kuzuia kusihi Sala; na imesemwa kuwa ni kila kitu anachokiona
uchafu mtu wa dasturi na akajikinga nacho na akasafisha nguo yake au/na mwili
wake kikimpata, kama vile choo kidogo au choo kikubwa.
Hukmu ya Kilichotoka Kwenye Tumbo la Mnyama
Vyenye kutoka kwenye tumbo la
mnyama vinagawika mafungu mawili:
La Kwanza, vile
ambavyo havikuwa kwa kutokana na kusagika tumboni, kama vile madenda na jasho
na mfano wa haya; haya hukmu yake ni hukmu ya mnyama wenyewe, ikiwa mnyama
wenyewe ni najsi, na haya ni najsi; ikiwa mnyama wenyewe ni 'taahir, na haya ni
'taahir.
La Pili, vile
ambavyo vimekuwa kwa kutokana na kusagika tumboni, kama vile choo kidogo, choo
kikubwa, damu, matapishi; hivi vyote ni najsi ikiwa vinatokana na mnyama
asieliwa. Choo kidogo (mkojo), kuwa ni najsi kumetolewa hoja kwa yule Bedui
aliekojowa msikitini; Mtume wetu Mpenzi s.a.w. akaamrisha umwagiwe doo la maji
huo mkojo. Na Hadithi ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w. kukhusu makaburi mawili,
alipopita Mtume wetu Mpenzi s.a.w. akaona wanavyo adhibiwa waliomo katika
makaburi mawili hayo, akasema s.a.w.:
"Ama mmoja wao alikuwa hajikingi na mkojo
wake". (Imehadithiwa na Muslim).
Ama amri ya Mtume wetu Mpenzi
s.a.w. ya kunywa mkojo wa ngamia, hivyo ilikuwa ni kwa ajili ya dawa; na
kujitibu kwa kitu najsi inajuzi iwapo kitakosekana kitu 'taahir ambacho
kitakuwa mahala pa kile najsi. Ama qauli ya Mtume wetu Mmpenzi s.a.w.:
"Hajajaalia Mwenyezi Mungu Mtukufu dawa
kwa umati wangu kwa kilicho haramishwa".
Imesemwa kuwa Hadithi hii
imekusudiwa juu ya ulevi. Ama kukhusu najisi ya choo kikubwa imekuja hoja yake
kwa qauli ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w.:
"Hakika utakosha nguo yako ikiingia choo
kidogo, choo kikubwa, madhii na matapishi". (Imehadithiwa na Ahmad na
Darqu'tny na Al Bazzaar).
Hadithi hii ni dalili ya kwamba
matapishi na madhii ni najsi. Madhii ni maji meupe mepesi yenye kuganda/kunata
hutoka bila ya matamanio kwa kuchezeana na kwa kutazama. Ama unajsi wa mavi ya
wanyama ni kwa qauli ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w. alipotaka kustanji akapelekewa
mawe mawili na donge la mavi makavu ya mnyama, akachukuwa s.a.w. yale mawe
mawili na akaacha kuchukuwa lile donge la mavi na akasema s.a.w.:
hili ni uchafu, na uchafu ni
najsi.
Ama unajsi wa wa
wadii ni kwa qauli ya Sayyidah 'Aisha r.a.:
Wadii,
ni maji meupe yenye uchafu na mazito
hutoka baada ya kukojoa au kwa kuchukuwa kitu kizito.
Ama unajsi wa damu umethibiti kwa
Qauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
Na kwa qauli ya Mtume wetu Mpenzi
s.a.w.:
"Jikoshe damu na usali".
Ama manii si najsi, sawa yakiwa ni
manii ya mwanamume au ya mwanamke. Manii ya mnyama, inategemea, ikiwa ni ya
mnyama ambae ni najsi, basi na manii yake ni najsi; ikiwa ni ya mnyama ambae si
najsi, basi na manii yake si najsi.
Kukosha Najsi
Kukosha kuiondoa najsi ni waajibu
kama ilivyokuja katika amri kama tulivyo tangulia kueleza. Ama namna ya kukosha
najsi kuna khitalifiana kwa kukhitalifiana najsi yenyewe. Ikiwa najsi yenye
kuonekana kwa macho, ni lazima katika kuikosha iondoke kwa dhati yake, na rangi
yake na ladha yake na harufu yake. Ikibakia ladha basi pahala ilipoingia hio
najsi hapatakuwa pame'tahirika. Ikibakia rangi ya najsi yenyewe na hali ya kuwa
si taabu kuondosheka, basi pahala ilipoingia hio najsi hapatakuwa
pame'tahirika. Ikiwa ni taabu kuondosheka, kama vile nguo kuingia damu ya
hedhi, basi hu'tahirika kwa vile kuwa ni taabu kuondosheka hio rangi ya damu.
Na ikiwa najsi itabakia harufu yake, kama vile harufu ya ulevi basi hu'tahirika
kwa vile ni taabu kuondosheka harufu ya ulevi. Ama najsi isio onekana kwa
macho, kama vile najsi ya maji-maji ambayo haina rangi; hii inapasa kukoshwa
kwa kusuguwa kwa nguvu mpaka iondoke, isipokuwa mkojo wa mtoto mchanga
mwanamume ambae hajala wala hajanywa isipokuwa maziwa ya mama yake, huu
utakoshwa kwa kurushiwa maji mpaka maji yazidi mkojo na kuenea sehemu yote
ilioingia mkojo, si lazima maji yachururike. Ama mkojo wa mtoto mchanga
mwanamke inapasa ukoshwe sawa na mkojo
wa mtumzima. Dalili ya tafauti hii, baina ya mkojo wa mtoto mchanga
mwanamume na mkojo wa mtoto mchanga mwanamke ni Hadithi ya Sayyidah 'Aisha r.a.
kuwa Mtume wetu Mpenzi s.a.w.:
"Mtume wetu Mpenzi s.a.w.
alipelekewa mtoto mchanga mwanamume, akakojoa kwenye pahala pake anapokaa
s.a.w., akataka aletewe maji, akamwagia kwenye hapo pahala wala hakupakosha, na
katika riwaya nyengine ni kuwa alinyunyizia maji juu yake; na katika riwaya
nyengine alirashia juu yake maji wala hakupakosha".
Muhimu ni kwamba riwaya zote hizi
zina maana moja, yaani Mtume wetu Mpenzi s.a.w. alimwagia maji kwenye mkoja wa
matoto mchanga mwanamume na wala hakukosha hapo pahala alipokojolea huyo mtoto.
Na kwa alivyo hadithia Imam Al Tirmidhy r.a. kuwa:
Na kutokana na Sayyidna 'Ali r.a.
kuwa amesema Mtume wetu Mpenzi s.a.w. kukhusu mkojo wa mtoto mchanga mwanamume
na mkojo wa mtoto mchanga mwanamke:
"(Mkojo wa mtoto mchanga mwanamume)
hurashiwa maji juu yake, na mkojo wa mtoto mchanga mwanamke hukoshwa".
(Imehadithiwa na Ahmad).
Ama mtoto mchanga mwanamume akila
chakula basi itabidi kukoshwa mkojo wake, sawa na mkojo wa mtoto mchanga
mwanamke. Mtoto mchanga mwanamke yeye mkojo wake unakoshwa, ikiwa analishwa au
hajalishwa.
Hii tafauti ya hukmu baina ya
mkojo wa mtoto mchanga mwanamke na mkojo wa mtoto mchanga mwanamume
imechukuliwa kwa kutizama ya kwamba mara nyingi watu huwa zaidi na watoto
wanaume kuliko watoto wanawake. Hivyo huwa mara nyingi wanawachukua na
kuwabeba, hivyo kuwepo uwezekano wa kupatwa na mkojo wao mara nyingi, kwa hivyo
ikajaaliwa wepesi katika ku'tahirisha mkojo wa watoto wachanga wanaume.
Hukmu ya Mnyama Anaekufa Kwenye Kitu Cha Maji-Maji
Mnyama akifa kwenye kitu cha
maji-maji, ikiwa ni maji, au mafuta, au samli au chakula, ikiwa huyo mnyama ni
mwenye damu ya kuchururika basi hunajsika hicho alichokufia ndani yake; hivi ni
kwa qauli ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w. alipoulizwa kuhusu panya akifa kwenye
samli, akasema s.a.w.:
Amri ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w.
ya kuimwaga hio samli ni dalili ya kuwa imenajisika hio samli. Ama ikiwa huyo
mnyama si mwenye damu ya kuchururika, kama vile nzi, mbu, nge, mende, sisimizi
na wa mfano wao; hawa wakifa kwenye maji au kitu cha maji-maji hakinajsiki.
Hivi ni kwa qauli yake Mtume wetu Mpenzi s.a.w.:
Amri ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w.
kumzamisha nzi ambae huenda akafa katika hicho kinywaji chetu ni dalili ya
kutokuwa najsi huyo nzi, na kama ni najsi basi Mtume wetu Mpenzi s.a.w.
asingaliamrisha kuzamishwa ndani ya kinywaji chetu. Vilevile kulinda vyombo
vyetu visiingiliwe na wadudu hawa ni taabu, hivyo ikasamehewa kuwa ni najsi.
Hukmu hii ni kwa sharti ya kwamba
hicho kilichoingiliwa na wadudu hawa hakijabadilika ladha, rangi au/na harufu
kwa vile kuingiliwa na wadudu hawa, kikibadilika, rangi, ladha au harufu; basi
hunajisika. Najsi isio onekana kwa macho, kwa uchache wake; kama vile cheche za
mkojo au uchafu wenye kuganda kwenye miguu ya nzi, hukmu yake ni kutokuwa najsi
kama ilivyo hukmu ya mnyama asiekuwa na damu yenye kuchururika, hivi ni kwa
vile ni taabu kujilinda navyo.
Hukumu ya Mnyama Wakati Yuhai
Asili ya wanyama ni 'taahir, kwani
wao wameumbwa kwa manufaa ya binaadam, kupatikana manufaa yao vyema ni kwa wao
kuwa ni 'taahir. Imetolewa hoja juu ya hili kwa Hadithi kukhusu paka, kwa qauli
ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w.:
"Hakika yao (paka) si najsi, kwani wao ni
wenye kupita baina yenu". (Imehadithiwa na Maimam watano wa Hadithi).
Wametolewa katika hukmu hii, mbwa
na nguruwe kwani wao ni najsi. Unajsi wa mbwa umetolewa hoja kwa qauli ya Mtume
wetu Mpenzi s.a.w.:
Qauli ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w.
ku'tahirika. Kuhitaji ku'tahirika hakuwi
isipokuwa baada ya kunajisika, hivi ikathibiti unajsi wa mdomo wa mbwa. Ikiwa
mdomo wake ni najsi na ndio sehemu safi mno katika mwili wake kwa vile kuuramba
mdomo wake kila mara, basi kuwa najsi mbwa wenyewe ni ndivyo zaidi. Ama unajsi
wa nguruwe ni kwa kuwa nguruwe ni mchafu zaidi ya mbwa. Vile vile Al Mawridy
ametolea hoja juu ya unajsi wa nguruwe kwa qauli ya Mwnyezi Mungu Mtukufu:
"………,
au nyama ya nguruwe, kwani hiyo ni uchafu; ……". (Al An'aam
: 145).
Hukmu ya Nyamafu
Nyamafu wote ni najsi kwa Qauli ya
Mwenyezi Mungu Mtukufu:
Na kuharimishwa kitu ambacho
hakina karama, wala madhara ni dalili ya unajsi wake, kwani kitu huharimishwa
ama kwa karama yake, kama vile kula maiti ya binaadam, au kwa madhara yake, au
kwa unajsi wake. Na nyamafu hana karama wala madhara kumla, kwani kwa dharura imeruhusiwa kula nyamafu, kama ilivyokuja kwa
Qauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
“…… Lakini
mwenye kushikwa na dharura, bila ya kutamani wala kupita mipaka, basi hakika
Mola wako Mlezi ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu”. (Al An'aam
: 145).
Kwa hivyo basi, imebakia unajsi
kuwa ndio sababu ya kuharimishwa nyamafu. Nyamafu ni yule ulie muondoka uhai
wake bila ya kuchinjwa Kisharia. Huingia katika hukmu hii mnyama asiejuzu
kuliwa hata kama atachinjwa, vilevile na mnyama anae chinjwa na mtu ambae si Muislam
wala si miongoni mwa (Watu wa Kitabu)
Hutolewa katika kundi la nyamafu, samaki,
panzi, nyembure na wa mfano wao, vile vile kumbikumbi; na binaadam, wote hawa
hawamo kwenye kundi la nyamafu.
Kutolewa samaki kwenye kundi na
nyamafu ni kwa qauli ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w. kukhusu bahari:
"Hio (bahari) ni 'taahir maji yake,
halali maiti wake". (Imehadithiwa na Maimam watano wa Hadithi).
Ama uhalali wa panzi na kutolewa
katika kundi la nyamafu ni kwa qauli ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w.:
Tumehalalishiwa nyamafu
(maiti) wawili: samaki na panzi". (Imehadithiwa na Ibnu Maajah na Al
Bayhaqy).
Ama binaadam kutolewa katika kundi
la nyamafu ni kwa qauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Na kwa
hakika tumewatukuza wanaadamu.........". (Al Israai
: 70).
Na huku kutukuzwa binaadam ndio
kumemuondolea kuwa miongoni mwa nyamafu, najsi; hukmu hii ni kwa maiti wote wa
binaadam, ikiwa ni Islam au Kafiri. Ama qauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"…… Hakika washirikina ni
najsi, ……". (Tawba
: 28).
Unajsi unaokusudiwa hapa ni unajsi
wa itikadi au kujiepusha nao kama tunavyo jiepusha na najsi, wala si unajsi ya
kiwiliwili, kwani ingalikuwa ni unajsi wa kiwiliwili ingaliwajibishwa kukikosha
anachokigusa au kujikosha tukigusana nao.
Ikiwa atachinjwa mnyama (mwenye
kuliwa) akakutikana tumboni mwake mtoto, basi inafaa kuliwa mtoto huyo wala
haihitaji kuchinjwa, kwani huku kuchinjwa mama kumetosheleza.
Ku'tahirisha Najsi ya Mbwa Na Nguruwe
Hu'tahirishwa chombo alichotia
mdomo au kikiramba mbwa au nguruwe kwa kukoshwa mara saba, moja ya mara saba
hizo ni kwa mchanga.
Kukhusu mbwa imetolewa dalili kwa
qauli ya Mtume wetu Mpenzi s.a.w.: "
"Mbwa akichovya mdomo katika chombo cha
mmoja wenu, kikosheni mara saba, mara ya mwanzo kati ya hizo saba iwe kwa
mchanga". (Imehadithiwa na Muslim).
Na kwa ilivyo hadithiwa na Al
Tirmidhy r.a.:
"Ya mwanzo ya mara hizo, au
moja ya mara hizo (iwe) kwa mchanga".
Ikiwa imethibiti kulazimika
kukosha najsi ya mbwa kwa kuchovya mdomo wake, au kukiramba chombo, yaani
kutokana na madenda yake; basi kulazimika kukosha najsi ya mbwa kama vile choo,
au matapishi, jasho na kadhaalika ni kulazimika zaidi. Hadithi hizi ni dalili
ya unajsi wa mbwa na kunajisika kile alichochovya mdomo wake ndani yake au
kukiramba, kwani lau kama si najsi; isingekuwa kuvimwaga viliomo kwenye vyombo
walivyochovya midomo yao. Kuvimwaga viliomo kwenye vyombo ni kupoteza mali, na
Uislam unakataza kupoteza mali, na kama si najsi basi Mtume wetu Mpenzi s.a.w.
asingalituamrisha kuvimwaga. Unajsi wa nguruwe umechukuliwa dalili kwa kiasi
cha mbwa, na kwa vile kuwa nguruwe ni mchafu zaidi kuliko mbwa, kutokana na huu
uchafu wake ndio tunakatazwa kuweka/kufuga nguruwe kwa hali yoyote ile, tafauti
na mbwa. Najsi ya nguruwe hu'tahirishwa kwa kuoshwa sawa na najsi nyengine.
Kuwajibishwa kukosha najsi ya mbwa mara saba - moja kwa mchanga kumekuja kwa
makusudio ya kuondoa ile tabia ya Waarabu hapo zamani ya kuchanganinyika sana
na mbwa wao.
Ku'tahirika Tembo (Ulevi) Kwa Kua Siki
Ku'tahirika vitu huwa ama kwa
kukoshwa, kwa kudabighiwa au kwa mchanga; haya tumetangulia kuyaeleza; na
huenda ikawa ku’tahirika kwa kugeuka, yaani kitu kutoka hali hii na kuwa katika
hali nyengine; kama vile tembo kugeuka siki. Tembo likigeuka siki huwa si
najsi, hivi ni kwa sababu unajsi wa tembo ni kwa vile kulevya (madhara), na kwa
kugeuka ikawa siki huondoka kulevya, kwa kuondoka kulevya; kumeondosha unajsi.
Wamekubaliana wanazuoni ya kwamba kugeuka kunako kusudiwa ni kugeuka wenyewe,
bila kugeuzwa; kugeuka kwa hali hii ndivyo hio siki haiwi najsi, huwa ni
'taahir. Ama ikiwa ni kwa kugeuzwa (si kugeuka wenyewe) kwa kutiwa vitu vya
kugeuzia, kama vile vitunguu au hamira, basi siki hio haiwi 'taahiri, bali huwa
najsi. Haya yametolewa dalili pale alipoulizwa Mtume wetu Mpenzi s.a.w. kama
tembo hufanywa siki, Mtume wetu Mpenzi s.a.w. akasema, halifanywi:
Maana ya Hadithi hii ni kama hivi:
"Ameulizwa (Mtume wetu Mpenzi s.a.w.)
kama tembo linafanywa siki akasema: Laa, yaani halifanywi". (Imehadithiwa
na Muslim).
Amekataza Mtume wetu Mpenzi s.a.w.
tembo kuligeuza siki kwa kutia ndani yake vitu vya kugeuzia, imetolewa dalili
ya kuharamishwa kufanya hivyo; kwamba:
Imekatazwa kulifanya tembo siki
kwa kutia vitu ndani yake kwa sababu vile vitu vitakavyotiwa ndani ya tembo
ambalo ni najsi, hunajsika kwa vile kuchanganyika na kitu najsi, yaani lile
tembo; kwa hivyo basi, litapogeuka hili tembo kuwa siki ile najsi ya vile vitu
vilivyotiwa kwenye tembo na kunajisika kwa kugusana na tembo, ambalo ni najsi,
vitainajisisha hii siki yenyewe, kwa hivyo hii siki itakuwa ni siki ilio najsi;
hivyo ndivyo ikaharimishwa tembo kuligeuza siki kwa kutia vitu ndani yake. Ama
likigeuka siki wenyewe bila ya kutiwa vitu, hivyo hufaa na hutumiwa hio siki
kuwa hali ya kuwa ni 'taahir, si najsi.
Kusamehewa Kutokana na Baadhi ya Najsi Kidogo
Zenye kusamehewa miongoni mwa
najsi kidogo kwa sababu ya shida ya kujikinga nazo ni:
Kwanza, tope za
njiani.
Pili, vile
ambavyo ni taabu kuviona kwa jicho la kawaida; kama vile cheche za mkojo,
tembo, vyenye kuganda miguuni mwa nzi, mende, wadudu wa kundi la sisimizi.
Tatu, damu ya
vidudu, kama vile kunguni, chawa na viroboto; na mavi ya ndege au ya mijusi
misikitini.
Nne, manyoya
kidogo ya wanyama wasioliwa (asipokuwa mbwa na nguruwe) na manyoya ya wanyama
wenye kupandwa kama punda, nyumbu, farasi.
Tano, moshi na
vumbi la najsi vinavyo peperushwa na upepo.
Sita, mnyama
najsi; kama vile mbwa akiingia kwenye maji yasiopita, kama vile kisimani au
ndani ya kidimbwi; na akatolewa kabla hajafa.
Saba, damu
inayobakia kwenye nyama au mifupa ya nyama inayojuzu kuliwa.
Nane, ikiwa
mnyama 'taahir kama vile paka; akitia mdomo kwenye kitu najsi, kisha akapotea
kwa muda na ikamkinika kuwa wakati alipopotea imewezakana kuwa katia mdomo wake
kwenye maji mengi, kama vile mtoni au kwenye kidimbwi cha maji, kisha akarejea
na akanywa maji kwenye chombo, basi hayo maji na hicho chombo havinajsiki.
Tisa, kamba
ikiwa itaanikiwa nguwo yenye najsi; baada ya muda ikikauka hio kamba kwa jua au
kwa upepo, basi inajuzu kuanikia nguo bila ya kukoshwa hio kamba wala
haitanajisisha nguo zinazoanikwa juu yake.
Kumi, mtu
akimwagikiwa na maji kutoka kwenye nyumba na hajui kama ni maji safi au si
safi, haimlazim kuuliza; atachukulia kuwa ni maji safi, isipokuwa akiona uchafu
kutokana na hayo maji. Hivi ni kwa hadithi iliotokea wakati wa Sayyidna 'Umar
r.a. kuwa yeye na sahibu wake walipita chini ya nyumba wakamwagikiwa na maji
kutoka mchirizini mwa nyumba hio. Sahibu yake Sayyidna 'Umar r.a. akamuuliza
mwenye nyumba kama ni maji 'taahir (safi) au si safi; Sayyidna 'Umar r.a.
akamwambia mwenye nyumba kuwa asiwambie, wakaendelea na safari yao.
Kumi na moja, maji/damu-damu
za chunusi; ikiwa kidogo zinasamehewa; ama ikiwa nyingi basi huwa ni najsi na
hunajisisha.
Kumi na mbili, ikiwa
mnyama anaekula na kuchakuwa baadae, kama vile n'gombe au mbuzi; ikiwa wakati
akichakuwa akanywa kwenye chombo hayanajisiki hayo maji wala hicho chombo
yaliomo hayo maji.
0 Comments